Ken Walibora ni miongoni mwa waandishi arifu na maarufu
zaidi wa fasihi ya Kiswahili waliowahi kuibuka katika Afrika
Mashariki na ya Kati. Mbinu ya kalamu yake ina mvuto
mkubwa na uzuri wa kisanaa wa aina yake. Ameziandika tanzu
mbalimbali za fasihi kama vile riwaya, ushairi na tamthilia.
Hata hivyo, Nasikia Sauti ya Mama ndiyo kazi yake ya
kwanza inayostahili kuitwa tawasifu, tawasifu inayoangazia
kipande kidogo halisi cha maisha yake mwenyewe na wala si
ya wahusika wake ambao ni zao la ubunifu.
Nasikia Sauti ya Mama ni tawasifu iliyosheheni mtindo wa
usimulizi wenye uwazi, ujasiri na umbuji. Uzuri wa kisanaa wa
tawasifu hii unashadidia ukweli usiokanushika kwamba
mwandishi huyu, aliyeibuka kwanza na riwaya ya Siku Njema,
ataendelea kutamba kwa miaka na mikaka katika medani ya
fasihi ya Kiswahili.